Source : Mwananchi
Posted by: Webmaster on 15-Dec-2009
RAIS wa Zanzibar Amani Karume, amesema urais wa visiwa hivyo sio wa watu wa Unguja pekee bali yeyote mwenye kutaka nafasi hiyo, awe ametoka Unguja au Pemba ana haki ya kuongoza.
Kauli ya Rais Karume inakuja siku moja baada ya kuchukua maamuzi ya kuwateua wawakilishi wawili kutoka Chama cha Wananchi (CUF) hatua ambayo imezidi kuleta mwanga wa kisiasa na maridhiano visiwani humo.
Akizidi kuonyesha azma yake ya kufuta makovu, chuki za kihistoria na dhana ya ubaguzi iliyojengeka kuhusu uongozi wa juu wa visiwa hivyo, Rais Karume alisema Zanzibar ni ya wote.
Rais Karume alitoa kauli hiyo juzi jioni katika hafla ya sherehe za elimu bila ya malipo, zilizofanyika katika Kijiji cha Vikunguni Mkoa wa Kusini Pemba.
Karume alihudhuria sherehe hizo kama sehemu ya ziara yake ya siku mbili kisiwani Pemba.
Zanzibar imekuwa ikitafunwa na historia ya U-Hizb na U-Afro Shiraz, tangu harakati za uhuru huku watu kutoka Unguja wakiona ndiyo wenye haki ya kutawala visiwa hivyo wakiona Wapemba kama wasaliti waliokuwa wakiunga mkono utawala wa Kisultan kabla ya mapinduzi ya Januari 12, 1964.
Lakini, katika kuonyesha kukwepa historia hiyo inayotafuna visiwa hivyo, Rais Karume alifafanua kwamba sio jambo la ajabu kwa mtu kutoka katika visiwa vya Pemba kupata fursa ya kuchaguliwa kuiongoza Zanzibar kwa kuwa suala la kuwa rais ni uamuzi wa wananchi wenyewe kumchagua mtu anayewafaa.
Hakuna kikwazo kwa mtu yeyote kuwa rais wa nchi hii wala msidhanie kwamba eti fulani tu ndie anayepaswa kuwa rais wa Zanzibar, hapana…mtu yeyote anaweza kuwa rais na mimi nakwambieni mtu anaweza akaukwaa urais nyote mkashangaa hapa,¯ alisema Rais Karume.
Kauli hiyo ya Rais Karume imeonekana kuwakera baadhi ya viongozi ambao kwa muda mrefu wamekuwa na mawazo ya kwamba, Zanzibar haiwezi kuongozwa na mtu kutoka Kisiwa cha Pemba hata akiwa anatoka CCM.
Baadhi ya viongozi wa CCM ingawa hawajawahi kuzungumza wazi wazi, lakini wamekuwa wakitoa kauli kama hizo jambo ambalo baadhi ya wana-CCM kutoka Pemba hujiona wanaonewa kutokana na kukoseshwa haki hiyo licha ya kuwa na uwezo.
Katika hatua nyingine, Rais Karume amewaita wachoyo wale wote wenye kuonyesha kukasirishwa na mazungumzo yake na Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad.
Kama mnahisi ni jambo baya basi huo ni uchoyo tena ni uchoyo, uchoyo sana tu, mimi nashangaa mbona nyingi huko mnashirikiana,¯alisema bila kufafanua
Wakati huohuo Exuper Kachenje na Boniface Meena wanaripoti kutoka Dar es Salaam kuwa, wanasiasa na wasomi wameipongeza hatua ya Rais Karume wa Zanzibar kuwateua wawakilishi wawili kutoka CUF huku Katibu, Uenezi na Sekretarieti ya CCM, John Chiligati akieleza huo ni mwanzo wa kuelekea kuundwa kwa Serikali ya Mseto visiwani humo.
Hatua ya Karume kuteua wawakilishi hao imekuja kipindi kifupi baada ya kufanya mazungumzo ya siri mara mbili na Katibu Mkuu wa CUF, huku ajenda zikiwa rohoni mwao.
Katibu Uenezi na Sekretarieti ya CCM, Chiligati, alisema: Sisi tumepokea kwa mtazamo chanya, ni maridhiano mazuri kwa hatima ya siasa za Zanzibar na ni ishara njema ya kuundwa kwa Serikali ya Mseto visiwani humo.¯
Akifafanua Chiligati alisema: CCM inabariki hilo kwa kuwa ni jema na ndiyo sera ya chama chake kutafuta na kupata maridhiano. Tunataka tujenge ushirikiano.
Akijibu swali ni vipi itawezekana kuundwa kwa Serikali ya Mseto wakati Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Zanzibar haziruhusu hilo, Chiligati alisema: Kwa Zanzibar hasa kwa sababu ya siasa za chuki, ili kuondoa siasa hizo za chuki hatuna tatizo na serikali ya ushirikiano kwani ndiyo njia ya kuondoa chuki.¯
Juzi Ikulu ya Zanzibar ilitangaza kuwa Rais Amani Karume amewateua Juma Haji Duni na Nassoro Mazrui kuwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.
Kwa upande wa Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Hamad Rashid Mohammed ambaye pia ni Mbunge wa Wawi (CUF), alisema chama chake kimepokea kwa furaha uteuzi huo huku akieleza umekuja katika wakati mzuri.
| On 17th Dec,2009 kinana wrote |
| Utumbu huo !tangu 64 baada ya mapinduzi mbona hatujayaona hayo,kuna nini karume hatuwapi wapemba serikali yetu. |

