Source : Ippmedia
Posted by: Webmaster on 02-Mar-2010
Abiria 39 pamoja na wafanyakazi saba waliokuwa wakisafiri na ndege ya shirika la ndege la ATCL aina ya Boeing 737 kutoka Dar es Salaam kwenda Mwanza jana walinusurika kufa baada ya ndege hiyo kuacha njia wakati ikitua katika uwanja wa ndege jijini Mwanza.
Kumekuwa na habari za kutatanisha juu ya chanzo cha ajali hiyo, huko baadhi ya vyanzo vya habari vikisema ni kuzima kwa injini, vingine ni kupasuka kwa tairi ya mbele ilhali vingine vikisema ni hali mbaya ya hewa.
Habari za kiuchunguzi zilizofanywa na mwandishi wetu jijini Mwanza zinasema kwamba wakati ndege hiyo ikitua tairi zake za mbele zilipata pancha na kuifanya kuacha njia huku bawa lake moja likiwa limebakia kwenye njia ya kutua.
Habari hizo zinasema kwamba ndege ikiwa tayari imekwisha kushika njia ya kutua, iliserereka umbali wa mita kadhaa na kuingia katika matope huku bawa lake moja likibaki kwenye njia.
Kamanda wa zimamoto kanda ya Ziwa, Juma Kwiyamba, alisema ndege hiyo yenye usajili namba 5H-MVZ ilipata ajali kati ya saa 1.40 na 1.45 asubuhi.
Kamanda huyo alisema chanzo cha ajali hiyo inawezekana kuwa ni hali ya hewa kwani wakati inatokea kulikuwa na mvua kubwa, ukungu pamoja na upepo mkali.
Naye Kaimu Meneja wa uwanja wa ndege wa jijini Mwanza, Byantao Muchunguzi, alisema kuwa wakati ndege hiyo ikitua tairi za mbele ziling’oka na hivyo kusababisha kuyumba na kwenda kwenye matope.
“Tunashukuru Mungu hakuna abiria aliyejeruhiwa, wote wametoka salama ila ni mishtuko midogo midogo,” alisema Muchunguzi.
Muchunguzi alisema kufuatia ajali hiyo uwanja huo umefungwa kwa muda usiojulikana hadi ndege hiyo itakapofanyiwa matengenezo na kuondoka.
Alisema kwa sasa wanasubiri wataalam kutoka Dar es Salaam kwa ajili ya kuchunguza chanzo cha ajali hiyo pamoja na kuifanyia matengenezo.
Hata hivyo, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Nonosius Komba, alisema wakati ndege hiyo ikitua uwanja ulikuwa umejaa maji hivyo kusababisha injini moja ya kulia kuzima.
Alifanunua kuwa baada ya injini kuzima ndege ilianza kuvutwa upande mmoja umbali wa mita 400 hadi kusimama.
Alisema ndege hiyo ilikuwa ikirushwa na rubani Joseph Ibanda akisaidiwa na rubani aliyejulikana kwa jina moja la Mwakang’ata.
Hali kadhalika, Ofisa Uhusiano wa Mamlaka ya Usalama wa Anga (TCAA), Abel Ngapemba, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo.
Ngapemba alifafanua kuwa ajali hiyo ilisababishwa na tairi za mbele kung’oka hali iliyosababisha ndege hiyo iyumbe na kunasa kwenye matope.
Mwishoni mwa wiki iliyopita ndege ya shirika hilo ilishindwa kutua na kulazimika kwenda uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kutokana na mvua kubwa iliyokuwa ikinyesha jijini Mwanza.
Wakati huo huo, abiria zaidi ya 120 waliokuwa wasafiri na shirika la ndege la Precision wamekwama kusafiri kutokana na uwanja wa ndege kufungwa kwa muda usiojulikana.
Kwa mujibu wa Ofisa Mauzo wa Shirika hilo, Hillary Edward, wengi wa abiria walikuwa wasafiri na Boeing kwenda jijini Dar es Salaam jana mchana.
“Tumelazimika kusitisha safari za ndege mbili baada ya uwanja kufungwa. Hata hivyo bado tunawasikiliza watalaamu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege kujua uwanja utafunguliwa lini,” alisema.
CHANZO: NIPASHE

